Friday, October 30, 2015

Kutangazwa rasmi mshindi wa urais 2015 kutokaa ukumbi wa Diamond Jubilee jijini Dar Es Salaam

Kutangazwa rasmi mshindi wa urais 2015 kutokaa ukumbi wa Diamond Jubilee jijini Dar Es Salaam,mh magufuri amepewa cheti.hafla hiyo iliyojumuisha watu mbalimbali wakiwemo jaji mkuu mstaafu mh warioba..na wasimamizi wa uchaguzi wa nje akiwemo mh rais wa nigeria obasanjo.

Thursday, October 29, 2015

Dr. John Pombe Magufuli (CCM) ametangazwa mshindi wa kiti cha Urais Tanzania 2015


Breaking Dr. John Pombe Magufuli (CCM) ametangazwa mshindi wa kiti cha Urais Tanzania 2015, kapata 58%, E. Lowassa 39%

TAARIFA YA CCM KWA VYOMBO VYA HABARI, OKTOBA 28, 2015


TAARIFA YA CCM KWA VYOMBO VYA HABARI, OKTOBA 28, 2015

 
CCM inapenda kutoa taarifa ifuatayo
kwa wana-CCM na kwa umma:
MALALAMIKO YA CCM KUHUSU
MATOKEO KWENYE BAADHI YA
MAJIMBO
Chama cha Mapinduzi hakijaridhishwa
na utaratibu wa kukusanya na
kujumlisha matokeo kwenye baadhi ya
majimbo. Katika majimbo manne
kumekuwa na ukiukwaji mkubwa wa
utaratibu wa uchaguzi, hasa katika
kujumlisha matokeo, uliopelekea
wabunge wa upinzani kutangazwa
washindi. Majimbo hayo ni Iringa
Mjini, Mikumi, Ndanda na Kawe.
Wasimamizi wa uchaguzi katika
majimbo haya wamevuruga uchaguzi.
Kutokana na utata uliokuwa
umejitokeza wakati wa zoezi la
kujumlisha kura, CCM iliomba kura
zihesabiwe upya lakini ikanyimwa haki
hiyo ya msingi ambayo iko kwenye
sheria. Kwenye baadhi ya majimbo,
ikiwemo Nyamagana, wapinzani
walipewa haki ya kura kuhesabiwa
upya. Kwa msingi huo, CCM imeamua
kwenda mahakamani kupinga matokeo
ya uchaguzi katika majimbo haya.
Tunataka sote tujiridhishe kwamba
utashi wa wananchi umeheshimiwa.
Bado tunaendelea kukusanya taarifa
za maeneo mengine kama kulikuwa na
ukiukwaji mkubwa uliobadilisha
matakwa ya wapiga kura. Hata hivyo,
tunakiri kwamba kwenye maeneo
mengi tulikopoteza viti vya Ubunge,
tumepoteza kihalali, hatuna
malalamiko, tunaheshimu maamuzi ya
wananchi, na tutafanya tathmini baada
ya uchaguzi ili tubaini makosa na
kuyarekebisha.
MAONI YA WAANGALIZI WA
UCHAGUZI
CCM imepokea maoni ya awali ya
waangalizi wa uchaguzi. Tumefarijika
kwamba karibu wote wametoa kauli ya
pamoja kwamba uchaguzi huu ulikuwa
wa haki na huru, uliofanyika kwa
uwazi na kwa amani – na kwamba
changamoto zilizojitokeza ni ndogo na
zimetokea katika maeneo machache
kiasi zisingeweza kubadilisha matokeo
ya uchaguzi yanayotangazwa sasa.
Tumepokea mapendekezo waliyoyatoa
kwa wadau mbalimbali kuhusu namna
ya kuboresha mchakato wa uchaguzi
kwa miaka ijayo, na hivyo kuimarisha
demokrasia nchini mwetu. Kwa kauli
za waangalizi hawa, kwamba, kwa jinsi
uchaguzi ulivyoendeshwa, matokeo
yanayotangazwa sasa ni kielelezo
sahihi cha utashi wa Watanzania
kuhusu viongozi wanaowataka.
MALALAMIKO YA UKAWA
Tumesikia malalamiko ya viongozi wa
UKAWA kupitia mkutano wao na
waandishi wa habari jana.
Tumeshangazwa na kauli kwamba
hawakubali matokeo ya Urais
yanayotangazwa na Tume. Hata hivyo,
matokeo ya Ubunge wanayakubali na,
kule wanakoshinda,
wanayasheherekea. Tunashangazwa
kwasababu
Tume iliyoandaa uchaguzi wa Rais ni
hiyo hiyo iliyoandaa uchaguzi wa
Wabunge, wasimamizi ni walewale,
vituo ni vilevile, na sheria na taratibu
zilizotumika ni zilezile. Hata fomu ya
matokeo walizosaini wakala wao
kwenye vituo vya kupiga kura,
zimegawanywa katika sehemu
(columns) tatu: Urais, Ubunge na
Udiwani. Mawakala wao walisaini
fomu hizo kwenye vituo vya kupiga
kura. Wameanza kuwa na matatizo na
matokeo haya baada ya kuona
mwelekeo wa kushindwa. Kama
mwelekeo ungekuwa tofauti,
wangekuwa na imani na Tume,
wasimamizi na taratibu zote.
Tunaomba ifike pahala sasa kwamba,
katika kuijenga demokrasia yetu na
kuliimarisha taifa letu, tuanze
utamaduni mpya wa anayeshindwa
kunyanyua simu kumpigia
anayeshinda na kumpongeza. Nafasi
ya mwisho aliyonayo Mgombea wa
UKAWA kuendelea kujijengea heshima
katika jamii yetu, na kuwa
mwanademokrasia, ni kwa kufanya
hivyo siku Dkt. Magufuli
atakapotangazwa mshindi.
Kwetu sisi CCM, kuchagua wagombea
bora na kuwanadi na kutengeneza sera
bora na kuzinadi, pamoja na rekodi
yetu katika uongozi wa nchi, ndio njia
zetu pekee za ushawishi. Katika
uchaguzi huu, wananchi wamefanya
maamuzi yao kwa uhuru na utashi,
ikiwemo kuwaangusha mawaziri sita
ambao tuliwasimamisha kama
wagombea wetu katika majimbo
mbalimbali. Nguvu na utashi wa
wananchi umejidhihirisha katika
uchaguzi huu.
Mchakato wa uchaguzi sasa unakaribia
kufikia ukingoni, tutawapata
madiwani, wabunge na Rais,
tunapaswa kuendelea na maisha na
tuwape nafasi watutumikie. Jitihada
tunazoziona sasa za viongozi wa
UKAWA za kuendeleza siasa za
uchaguzi kwenye mitaa ya miji yetu
kwa njia za vurugu na maandamano
hazikubaliki hata kidogo. Tunalaani
kitendo cha wafuasi wa UKAWA
kuchoma ofisi za CCM katika Wilaya ya
Mbozi.
Amani ya nchi hii ina thamani kuliko
hitaji la madaraka la mtu yoyote.
Wenzetu wa UKAWA wana haki ya
kulalamika lakini hawana haki ya
kuiingiza nchi yetu machafukoni kwa
kuwakusanya vijana na kuwaingiza
mitaani wafanye vurugu na
kuhatarisha maisha, kuharibu mali na
kusimamisha shughuli za watu
wengine.
Tunawaomba Watanzania waendelee
na shughuli zao kama kawaida huku
kila mmoja akitambua wajibu wake wa
kuilinda amani ya nchi yetu.
January Makamba
Mjumbe wa Kamati ya Kampeni ya
CCM
28.10.2015 






Wednesday, October 28, 2015

Uchaguzi wa Zanzibar wafutwa


Mwenyekiti wa tume ya taifa ya uchaguzi zanzibar (zec) jecha salim jecha ametangaza kufutwa kwa uchaguzi wa wa serikali ya mapinduzi zanzibar kwahiyo uchaguzi utafanyika baada ya siku 90.

Wednesday, October 14, 2015

Wanafunzi wa vyuo-NEC


 TUME ya taifa ya Uchaguzi sasa imethibitisha
kuwa wanafunzi wa Vyuo vikuu hawatapiga
kura katika uchaguzi mkuu ujao.
Akizungumza katika kipindi cha kikaangoni
kinachorushwa na EATV, jana Emmanuel
Kawishe amesema kuwa wanafunzi hao
hawataweza kupiga kura kuchagua
diwani,mbunge au Rais kwa kuwa sheria
inasema kila mtu atapiga kura pale
alipojiandikishia.
“Sheria ya uchaguzi kifungu cha 61(3)a
kuwa kila aliyejiandikisha atapiga kura
alipojiandikisha” alisema Kawishe.
Aidha amefafanua kuwa vituo vyote vya kupigia
kura vitafunguliwa saa 1 asubuhi na vitafungwa
saa kumi jioni hivyo kuwatahadharisha wapiga
kura wote kuwepo kituoni kabla muda wa
kufunga.
Taarifa ya kutopiga kura kwa wanafunzi wa
vyuo vikuu imekuwa rasmi huku viongozi wa
Wanafunzi vyuo vikuu wakihangaika kupeleka
shauri mahakamani ili serikali ifungue vyuo
kwa wakati na kuwapa wao fursa ya kupiga
kura.
Hii ni mara ya pili kwa Vyuo vikuu kufunguliwa
baada ya Oktoba, kwa mara ya kwanza
ilifanyika vile vile mwaka 2010 kwa kisingizio
cha mikopo ya Elimu ya juu.
Ushahidi kutoka kwa wanafunzi mbalimbali
waliowahi kunufaika na mikopo wanasema
serikali haijawahi kutoa mikopo kwa wakati
licha ya sababu za mara kwa mara kuahirisha
kufungua vyuo wakati wa Uchaguzi.
Mapema mwaka huu, Shirikisho la wanafunzi
wa wanachadema wa Vyuo vikuu (Chaso)
kupitia Kaimu Mratibu wao Wilfred
Mwalusanya aliitaka NEC kueleza utaratibu wa
kuwaandisha wanavyuo ili wakati wa kupiga
kura waweze kushiriki.
Tayari tuhuma zimeanza kutolewa na wadau
mbalimbali kuwa tume imetumiwa na serikali
ya CCM ili kuinusuru sababu wanavyuo
wamehamasika kuelekea uchaguzi mkuu mwaka
huu. 

TAMKO RASMI LA BALOZI JUMA V. MWAPACHU.


TAMKO RASMI LA BALOZI JUMA V. MWAPACHU. NAJIVUA UANACHAMA WA CCM

Ndugu zangu,
Kesho ni siku muhimu katika kalenda ya Taifa
letu. Tunamkumbuka marehemu Baba wa Taifa,
Mwalimu Julius Kambarage Nyerere aliyetutoka
miaka 16 iliyopita. Nadhani ni siku mwafaka
kwangu kufanya maamuzi magumu katika
maisha yangu ambayo yanahusu uanasiasa
wangu. Mimi ni mwanachama wa CCM tangu
mwaka 1967 wakati nilipojiunga na TANU
Youth League. Nimepata fursa ya kuwa
kiongozi ndani ya Chama hiki. Lakini kuanzia
kesho mimi si mwanachama wa CCM tena.
Natoa maelezo yafuatayo:
Kwa kipindi chapata mwezi na nusu hivi sasa
mmekuwa mkisoma makala zangu kuhusu
msimamo na mwelekeo wangu katika masuala
ya siasa za hapa nchini hususan kuhusu
uchaguzi mkuu na mstakabali wa demokrasia
nchini mwetu. Nyote mnatambua kwamba
kuanzia mchakato wa kumpata mgombe wa
Urais ndani ya CCM kule Dodoma, ambako
nilipiga kambi, sijayumba katika msimamo
wangu kwamba Edward Ngoyai Lowassa ndiye
chaguo langu katika kampeni za kumpata Rais
mpya wa Taifa letu.
Chaguo langu si ndoto wala mlipuko wa
mapenzi juu ya Lowassa.
Nimemfahamu Lowassa tangu miaka ya 90
nikiwa cadre wa Chama cha Mapinduzi kwa
mahusisho katika majukumu ya Kic,ssa amejaaliwa nuru na uwezo wa
kuongoza na wa kupendwa na watu. Ni msikivu
pamoja na kwamba ni kiongozi asiyependa
ukiritimba na utovu wa nidhamu, iwe kwa
upande wa watumishi au wananchi wenyewe.
Kubwa kwake ni ucha Mungu wake ambao
unamsaidia sana katika uongozi unaojali na
kuheshimu utu, ukweli na uwazi. Wanaodhani
au kutaharuki kwamba eti anaweza au ana
hulka ya kulipiza kisasi kwa jambo lolote lile ni
waongo; wanajilinda.
Lowassa ni chaguo la wengi na CCM, katika
busara yake ya kumuengua katika mchakato wa
kumpata mgombea wa Urais, kimedhihirisha
kutokuwa Chama kinachoendeshwa kwa misingi
ya demokrasia. Dalili za Chama hiki kupoteza
lengo la kuwa Chama cha watu, na kuwa cha
viongozi wachache zilianza siku nyingi na hasa
katika kipindi cha uongozi wa Mheshimiwa
Jakaya Mrisho Kikwete. CCM kimebadilika na
kuwa Chama cha makundi na migawanyiko
yakupambana, si kwa malengo ya itikadi na
ujenzi wa Chama, bali ya kumalizana na kutaka
kufukuzana.
Lowassa angeweza kufukuzwa miaka mingi tu
iliyopita! Aliweza kushinda vita hivyo kutokana
na kupendwa na wengi ndani ya CCM. Hivyo,
kujitoa kwake uanachama wa CCM hivi karibuni
ni sahihi kabisa kwasababu CCM si Chama tena
cha watu. Kimetekwa. Na mimi nakubaliana na
msimamo wa Lowassa na hao waliyofuata
kutoka nadani ya CCM.
Niliwahi kuandika makala katika ukurasa huu
nikimnukuu mshairi mmoja wa Uingereza
aliyeandika kwamba, ‘there comes a time when
the door opens and allows the future in’.
Mlango huo sasa umefunguka usoni mwangu na
huu uamuzi wangu maana yake ni kukubali
kwamba wakati mpya umewadia; ni wakati wa
mabadiliko. Kuendelea kujihisi kwamba ningali
mwana CCM wa kadi ni kukubali kujidanganya
mwenyewe. Si sawa. Kama marehemu Baba wa
Taifa alivyowahi kusema, ‘CCM si mama yangu’.
Hivyo ndugu zangu, kuanzia kesho mimi si
mwana CCM tena. Nitarejesha rasmi kadi yangu
kupitia ofisi ya CCM ya kata yangu Mikocheni,
Dar-es-Salaam. Kwa sasa sijaamua kujiunga na
Chama kingine.
Mwenyezi Mungu anilinde. 

Thursday, October 08, 2015

Bado masaa kadhaa Fainali ya BSS..


FAINALI YA BSS ITAFANYIKA KESHO KWA MUJIBU WA VIONGOZI WA BSS


Madam Ritha akiwatambulisha washiriki.
SHINDANO la kusaka vipaji vya muziki, Bongo Star Search (BSS) linalotarajiwa kufanyika Oktoba 9, limeongeza  zawadi ya mshindi wa shindano hilo  ambapo sasa atajinyakulia shilingi milioni 60,  ambapo shilingi milioni kumi zitapelekwa studio kwa ajili ya kusaidia shughuli za kurekodi.
Akizungumza mbele ya waandishi wa habari,  Jaji Mkuu wa shindano hilo Ritha Paulsen ‘Madam Ritha’, alisema kuwa shindano hilo lina  msisimuko wa kipekee kwa kuwa washiriki wote ni wazuri kiasi majaji wanapata wakati mgumu kumchagua  mshindi.
“Mshindi wa shindano hili ataondoka na sh. milioni 60, katika kinyang’anyiro cha safari hii chenye  msisimko mkubwa hadi hata sisi wenyewe tunapata wakati mgumu kama majaji,” alisema Ritha
Fainali za shindano hilo zinatarajiwa kufanyika Ijumaa Oktoba 9 Mwaka huu  katika Ukumbi wa King Solomon  uliopo eneo la Namanga Kinondoni jijini Dar es Salaam.  Siku hiyo pia kutakuwa na burudani za nguvu kutoka kwa msanii Run Town wa Nigeria ambaye kwa sasa anatamba na wimbo wake wa Gallardo.
“Ukiachia mbali msanii huyo pia kutakuwa na burudani kutoka kwa Christian Bella, Yamoto Bendi, Nevy Kenzo ambao watakamua sambamba na wasanii mahiri ambao ni zao la BSS kama Peter Msechu na Kala Jeremiah.  Viingilio siku hiyo vitakuwa 25,000/=, ambapo nafasi za VIP zitakuwa 50,000/= na viti maalum vitalipiwa 100,000/=.  Nawaomba mashabiki waje kwa wingi maana fainali ya mwaka huu ni ya kipekee kabisa,” alisema Madam Ritha.
Angel kato mshiriki katika fainali ya bss




Frida amani mshiriki wa Fainali ya BSS





Nasibu fonabo mshiriki wa Fainali ya bss

maelfu wajitokeza kumuaga Mchungaji Mtikila


RAIS Jakaya Kikwete ameongoza mamia ya waombolezaji pamoja na viongozi wa kitaifa, katika kumuaga Mwenyekiti wa Chama cha DP, Mchungaji Christopher Mtikila aliyekufa kwa ajali hivi karibuni mkoani Pwani.
Katika shughuli hiyo, viongozi wengi waliohudhuria walimuelezea Mtikila kuwa ni mwanaharakati wa mageuzi, aliyeipigania Tanganyika mpaka kifo chake, lakini pia alisimamia na kuheshimu taratibu za kisheria na kutaka mabadiliko bila uoga.
Rais Kikwete alifika katika shughuli hiyo ya kumuaga Mtikila iliyofanyika jijini Dar es Salaam jana, akiambatana na Makamu wa Rais, Dk Mohammed Gharib Bilal na Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, William Lukuvi.
Viongozi wengine waliohudhuria shughuli hiyo ni Makamu wa Kwanza wa Rais Zanzibar, Maalim Seif Sharif Hamad ambaye pia ni Katibu Mkuu wa Chama cha Wananchi (CUF), Msajili wa Vyama vya Siasa, Jaji Francis Mutungi, Msajili wa zamani wa vyama hivyo, John Tendwa na Makamu Mwenyekiti wa CCM (Bara), Philip Mangula.
Pia walikuwepo Mwenyekiti wa Baraza la Vyama vya Siasa, Peter Mziray ambaye ni Mwenyekiti wa chama cha PPT-Maendeleo, Makamu Mwenyekiti wa Chadema, Profesa Abdallah Safari na Naibu Katibu Mkuu wa TLP, Dotnata Rwechungura.
Akizungumza katika shughuli hiyo ya kumuaga Mtikila ambaye jeneza lake lilifunikwa kwa bendera ya Tanganyika, Msajili wa Vyama vya Siasa, Mutungi aliwataka watanzania kumuenzi mchungaji huyo kwa matendo yake ya kuchukia vurugu na badala yake aliamini zaidi katika sheria.
“Mchungaji Mtikila atakumbukwa kwa misimamo yake mikali. Alipenda kusimamia kile anachokiamini. Lakini kubwa zaidi alitoa mchango katika nyanja ya Sheria, kwa sasa huwezi kuzungumzia masuala ya sheria hususani haki za binadamu bila kumtaja Mtikila,” alisema Mutungi.
Alisema kupitia sekta ya Sheria, mwanaharakati huyo alifanikisha mabadiliko kadhaa, ikiwemo kuingizwa kwenye Katiba kwa kifungu kinachoruhusu mgombea binafsi, lakini pia alifanikisha kubadilishwa kwa kifungu kinachohusu maandamano.
“Huyu alikuwa ni mpambanaji, alifungua kesi nyingi kwa kuwa aliamini katika kufuata sheria na si kuandamana au kufanya vurugu. Naomba tumuenzi kwa kutopenda kushinikiza fujo na maandamano, vyombo vya sheria vipo kama kuna tatizo tuvitumie kutafuta haki,” alisisitiza.
Kwa upande wake, Dk Bilal alimtaja Mchungaji Mtikila kuwa alikuwa ni mtu jasiri, aliyeshirikiana na wenzake bila kujali tofauti za mitazamo waliyonayo. “Mimi nilimfahamu Mtikila kupitia uanaharakati wake wa kutaka mabadiliko, ni kweli alikuwa anataka sana kuirejesha Tanganyika, lakini pamoja na tofauti za fikra zetu, alikuwa anakuja hadi ofisini kwangu kipindi kile nilikuwa Katibu Mkuu Wizara ya Sayansi, Mawasiliano na Teknolojia na tulikuwa tunazungumza sana,” alisema.
Aliwataka watanzania kuiga mfano wa matendo ya Mtikila, kwani kwa sasa nchi inataka watu kama hao wenye mawazo mapya na hawaogopi kuyatoa na kuyatetea bila kudharau mawazo na fikra za wengine.
Maalim Seif, kwa upande wake, alisema alifahamiana na Mtikila kupitia harakati zake za kisiasa na kubainisha kuwa ni mtu anayejiamini, asiye uoga na mwenye kuajimini na kusimamia kile anachokiamini.
Mziray alisema anaipongeza Serikali kwa kitendo chake cha kushirikiana na familia ya Mtikila kwa hali na mali, bila kujadili kuwa ni mwanaharakati wa mabadiliko, jambo alilosisitiza kuwa hiyo ndio Tanzania inayotakiwa kwa sasa.
Makamu Mwenyekiti wa DP, Peter Mwagila alibainisha kuwa chama hicho kimepata pigo na pengo kubwa kwa kuondokewa na mwenyekiti wao, ambaye pia pamoja na kuwa muasisi wa chama hicho, ni mwanaharakati wa mageuzi aliyepigania nchi yake ya Tanganyika.
“Mtikila ndoto zake zilikuwa ni kurejeshwa kwa Tanganyika ambayo iliondolewa kwenye ramani ya dunia tangu mwaka 1962, alitaka kuwepo na Rais wa Tanganyika, Katiba, wabunge na mamlaka zote za nchi ya Tanganyika. Lakini pia alipinga rushwa, ufisaidi na kuwachukia viongozi wanaojilimbikizia mali,” alisema.
Alisema chama hicho kitahakikisha kinaendeleza na kusimamia harakati zote zilizoanzishwa na Mtikila ikiwemo kuidai Tanganyika. Msemaji wa familia ya mchungaji huyo, Peter Mayani, wakati akisoma wasifu wa Mtikila, alisema mwanaharakati huyo alibobea katika fani za sheria, uchumi na masoko na aliwahi kuajiriwa Mahakama Kuu na Shirika la Ndege la Afrika Mashariki, ambalo alilitumia kutoroshea wanaharakati wa chama cha Frelimo.
Alisema Mtikila aliokoka rasmi mwaka 1983 na kuanzisha Kanisa la Pentekoste la Full Salvation na mwaka 1990 alianza harakati za ukombozi, zilizoshinikiza kuanzishwa kwa vyama vingi mwaka 1992. Pia alianzisha chama cha DP, ambacho kilichelewa kupata usajili wake hadi mwaka 2000.
Mtikila baada ya kuagwa alisafirishwa kwenda kijijini kwao Milo, wilayani Ludewa mkoani Njombe ambako anatarajiwa kuzikwa leo. Marehemu ameacha mjane Georgia Mtikila. Askofu wa Kanisa la Ufunuo, Nabii Paul Bendera, aliwataka watanzania kutambua kuwa wote ni wageni duniani na kwamba kila mtu bila kujali ni nani duniani na ana cheo gani iko siku yake atakufa.
“Kwa sasa hali imekuwa ngumu na mbaya nawaomba ndugu zangu tuwe makini, lakini kubwa zaidi kila mtu amheshimu maisha ya mwenzake tuweke upendo na amani mbele na hii iwe ndio kipaumbele chetu. Naomba Serikali nayo iongeze juhudi za kuwalinda wananchi wake,” alisisitiza.
Mchungaji Daudi Mwaijojele, alitumia fursa hiyo kuwataka watanzania kuacha uchafu na kumrejea Mungu, ili kutengeneza maisha yao ya baadaye pindi watakapokufa. “Nawaomba acheni uchangudua, ufisadi na michepuko tena hiyo michepuko ndio inaleta magonjwa kama vile Ukimwi majumbwani na kusambaratisha familia,” alisema.
Mtikila alikufa kwa ajali ya gari aina ya Toyota Corolla, lenye namba za usajili T 189 AGM maeneo ya Msolwa wilayani Bagamoyo, mkoani Pwani. Alikuwa akitokea Njombe kwenda Dar es Salaam.